Dar es Salaam. Baadhi ya wabunge wa Chadema wamezungumzia taarifa zinazosambaa zikieleza kuwapo mkakati wa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kuhamia katika chama hicho, wengi wao wakimkaribisha.
Wakati wabunge hao wakikubali kumpokea,
 Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa amesema wananchi wasubiri
 mambo yatakapokuwa tayari badala ya kutegemea mitandao ya kijamii.
“Nitazungumza
 pale mambo yatakapokuwa sawa, siwezi kuzungumza sasa, subirini… sasa 
hivi mambo mengi yanazungumzwa kwenye mitandao,” alisema Dk Slaa ambaye 
pia anatajwa kuwa mgombea wa chama hicho ndani ya Ukawa.
Msemaji
 wa Lowassa, Aboubakary Liongo alipoulizwa kuhusu kuwapo kwa mpango huo 
alisema hawezi kulizungumzia hilo kwa kuwa ni suala la mtu binafsi. Hata
 hivyo, jitihada za kumpata Lowassa jana hazikufanikiwa kwani simu yake 
iliita pasi na kupokewa.
Hivi karibuni, idadi kubwa ya 
madiwani wa CCM walirudisha kadi zao na kujiunga na Chadema wakisema 
sababu ni kutoridhishwa na kukatwa kwa jina Lowassa kati ya wagombea 
urais wa CCM.
Kadhalika, mtandao wa kijamii uliokuwa 
ukimuunga mkono mbunge huyo wa Monduli unajulikana kwa jina la 4U 
Movement ulitangaza kuhamia Chadema hali inayoashiria kuwa kuna dalili 
ya Lowassa pia kujiunga nao.
Wakiandika katika akaunti 
ya Twitter ya 4U Movement, wafuasi hao walisema: “Ukimya ni hekima na 
ukimya ni busara. Ukimya wa Edward Lowassa ni kutafakari Safari ya 
Matumaini... Tuungane kuyapata mabadiliko nje CCM.”
Chadema ni kanisa la wokovu
Akizungumzia
 taarifa hizo, Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa 
alikifananisha chama hicho na kanisa ambalo kwa kawaida halikatai mtu, 
bali linawapokea wenye dhambi na kuwaongoza kufanya toba.
“Chadema
 ni kama kanisa, hakataliwi mtu, tunahubiri habari njema ya wokovu, 
ukija hapa unatubu unaendelea kufanya kazi,” alisema.
Kuhusu
 viongozi wa CCM kuhamia Chadema, Msigwa alisema inawezekana kasi hiyo 
inachagizwa na Lowassa kukosa nafasi aliyoitaka ndani ya chama hicho.
“Unapokuwa
 mwanasiasa unakuwa na wafuasi, inawezekana wengine wanaohamia Chadema 
ni watu wake ambao wameona mtu wao amekosa nafasi aliyoitaka ndiyo maana
 wanakihama chama,” alisema.
Msigwa alisema Chadema 
ilikuwa inakusanya wanachama wapya kwa muda mrefu hata kabla ya vuguvugu
 la Lowassa na chama chake kuibuka na ushindi na wanaohamia wanafanya 
hivyo kwa sababu wanakipenda chama na wameichoka CCM.
Huenda akatimiza safari ya matumaini
Akizungumzia
 ujio wa Lowassa kwenye chama hicho, Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless 
Lema alisema iwapo Lowassa atahamia Chadema anakaribishwa na huenda 
akaitimiza safari yake ya matumaini.
“Namkaribisha Lowassa Chadema, huenda safari yake ya matumaini ikaishia huku, akawa mwanachama au hata kiongozi,” alisema.
Alisema
 hakuna shaka kuwa mbunge huyo wa Monduli ana nguvu ndani ya CCM ndiyo 
maana viongozi wengi wa chama hicho wanakihama wakati huu.
“Hiyo
 ilijionyesha kuanzia kwenye Kamati Kuu ya CCM, Halmashauri Kuu, Lowasa 
amekamata wajumbe kwa asilimia 80 na hiyo ni ishara kuwa ameishika CCM,”
 alisema.
Lema aliongeza kuwa wanaoihama CCM hawaihami kwa bahati mbaya, bali wameona mtu wao waliyemtarajia ameondoka.
“Ni
 wengi wanaohamia Chadema, kwa sasa kadi zimetuishia na hiyo ni ishara 
kuwa CCM inakufa, ripoti za mikoa yote tunazo,” alisema.
Mbunge
 wa Viti Maalumu, Lucy Owenya alisema  wanaoihama CCM kwa sasa 
wamegundua kuwa chama pekee kinachoweza kutetea wananchi ni Chadema.
“Sisi
 tunawakaribisha kwa mikono miwili, waje tuchape kazi, ilimradi 
wanafuata kanuni na taratibu za chama, basi.  Wamejionea wenyewe kuwa 
CCM hakuna chochote,” alisema.
 Alisema CCM waliamua 
kupitisha katiba bila kuwapo kwa Ukawa, lakini sasa wameona kuwa 
walichokifanya ni makosa na wameanza kurudi Chadema ambako wanaamini 
kuna demokrasia ya kweli.
Mbunge wa Viti Maalumu, 
Cecilia Paresso alisema: “Tunamkaribisha kwa mikono miwili. 
Tumekinyooshea CCM vidole kwa muda mrefu kuwa kuna rushwa na makundi na 
hilo linajidhihirisha sasa. Lakini wale wote wanaokuja Chadema, 
tunawakaribisha ili mradi wafuate kanuni na taratibu zetu.”
Paresso
 alisema hana tathmini ya kina kuhusu wafuasi wa Lowassa wanaoihama CCM,
 bali wanaokihama chama hicho wameona kina matatizo.
Atakiwa akidhi vigezo na masharti
Licha
 ya kuonyesha kumkaribisha, katika chama hicho, baadhi ya wabunge 
walimtaka Lowassa afuate kanuni ili awe mwanachama mwenye sifa.
Mbunge
 wa Mbozi Magharibi, David Silinde alisema anakaribishwa lakini hana 
budi kufuata sheria na kanuni za chama... “Anatakiwa afuate taratibu za 
chama, milango ipo huru, lakini afuate kanuni… asije akafikiri ataleta 
taratibu zake hapa, sitakubali.”
Silinde alisema 
wanaohamia Chadema hawajapendezwa na mwenendo mzima wa uteuzi wa mgombea
 wa urais na hivyo wameifuata demokrasia ya kweli ndani ya chama hicho.
Mbunge
 wa Kawe, Halima Mdee hakutaka kuzungumzia kwa undani suala hilo lakini 
alisema endapo atajiunga, chama hicho kitampokea kulingana na vigezo na 
taratibu.
“Akihamia Chadema nitatoa maoni yangu lakini 
ninachoweza kusema ni kuwa kila mtu ana haki ya kwenda chama chochote 
ili mradi ana tija,” alisema.
Mdee alisema wanaCCM wanaohamia Chadema wamesoma alama za nyakati na kuona kuwa CCM haiendani na ahadi zake.
Mbunge
 wa Viti Maalumu, Susan Lyimo alisema, Lowassa ni binadamu wa kawaida 
kwa hiyo kuhamia kwake Chadema si kitu cha ajabu ilimradi afuate 
kanuni... “Cha muhimu afuate masharti ya chama, kanuni na  taratibu, 
kama watu wanahama vyama vingine yeye ni nani asihame CCM?”
Lyimo alisema wanaCCM wengine wanakaribishwa kujiunga kwa sababu kwenye siasa hakuna rafiki wa kudumu wala adui wa kudumu.
Mbunge
 wa Viti Maalumu, Pauline Gekul, aliwataka wana CCM na Lowasa kuhamia 
zaidi  Chadema ili kuunganisha nguvu na kuichukua nchi.
 “Mfikishie salamu Lowassa mwambie karibu kwenye jeshi la ukombozi,” alisema.
Katibu wa CCM amuonya
Akizungumza
 na waandishi wa habari jana katika Ofisi za CCM Mkoa wa Dodoma, Katibu 
wa CCM mkoa huo, Albert Mgumba alisema ingawa kuhama chama ni hiari ya 
mtu, Lowassa hapaswi kuchukua uamuzi wa hasira kiasi hicho badala yake 
awe mstari wa mbele kuhamasisha umoja ndani ya chama.
Alimtaka
 kutothubutu kuihama CCM na endapo afanya uamuzi huo atambue kuwa hawezi
 kukisababishia pengo lolote zaidi ya kujipunguzia hadhi yake ya 
kisiasa.
“Mgombea tuliyempata sasa ni makini kuliko, anapendwa, utendaji wake unajulikana kila mahali,” alisema Mgumba.
Endelea hapa====>>>>>
Endelea hapa====>>>>>

0 Comments
Unapenda kuhabarika? Jiunge nasi Katika Twitter na Facebook ili tuhabarishane.
Kumbuka Kuacha maoni yako hapa pindi usomapo habari zetu. Karibu Tena