Header Ads Widget

Responsive Advertisement

FAHAMU | Faida 6 Utakazopata Pale Utakapowafundisha Watu Kile Unachokifahamu

Image result for teaching
Sio watu wengi wanaopenda au wanafahamu umuhimu wa kuwafundisha watu wengine kile wanachokifahamu. Wengi huona kuwa kufundisha watu wengine ni kazi duni ambayo haiwezi kuwanufaisha kwa njia yoyote ile.
Ukweli ni kuwa kufundisha watu wengine ni swala lenye manufaa mengi ambayo watu wasiofanya hivyo wanayakosa. Ikiwa unapenda kuwa bora zaidi pamoja na kuongeza maarifa yako, basi karibu nikufahamishe faida 6 za kufundisha watu wengine.

1. Hukuongezea maarifa

“Mwalimu ni mwanafunzi wa kudumu.”
Kufundisha wengine ni njia bora ya kuongeza maarifa yako. Kwanza kabisa utahitajika kujiandaa kwa kusoma na kujifunza mambo mbalimbali ili uweze kufundisha vyema, hili litakuongezea kiwango kikubwa cha maarifa.
Pili wakati wa kufundisha utajifunza mambo mbalimbali kutoka kwa yule unayemfundisha au wale unaowafundisha kwani nao kuna mambo wanayoyafahamu tofauti na wewe.

2. Hukufundisha kupanga na kuandaa

Ili uweze kufundisha vyema ni lazima upangilie na kuandaa kile utakachofundisha. Kwa njia hii utajifunza kupanga na kuandalia somo au mada yako kabla ya kuiwasilisha.

3. Buboresha uwezo wako wa mawasiliano

Utahitaji kuwasiliana na wale unaowafundisha ili wapate kile unacholenga kuwafundisha. Kwa njia hii utaboresha uwezo wako wa kuwasiliana.
Hili linahusisha pia kuboresha uwezo wako wa uandishi pamoja na uwezo wa kuzungumza mbele za watu ikiwa utakuwa unafundisha ana kwa ana.

4. Huwezesha kujitathimini

Njia bora ya kujitathimini ni kwa kufundisha watu wengine kile unachokijua kisha uwaruhusu wakupe tathimini ya uwezo wako.
Kwa njia hii utatambua ni jambo gani unalolifanya kwa ubora na ni wapi unapofanya kwa udhaifu ili ufanye maboresho zaidi.

5. Hukuwezesha kutatua matatizo ya watu

Kuwafundisha watu mambo mbalimbali ni njia bora na ya gharama nafuu ya kutatua matatizo yao. Hebu fikiri unamfundisha mtu jinsi ya kujikinga au kutibu maradhi fulani, akifanyia kazi maarifa hayo na kuona matokeo tayari utakuwa umetatua tatizo lake.
Kwa mfano pia unaweza kumfundisha mtu jinsi ya kujikwamua kiuchumi na akatoka kwenye matatizo ya kifedha; kwa njia hii utakuwa umefanya jambo kubwa kuliko hata kumpa pesa.

6. Hukutengenezea kumbukumbu muhimu

Ni vigumu sana kwa mwanafunzi kumsahau yule aliyemfundisha. Hili hujenga mahusiano na kumbukumbu nzuri kati yako na yule uliyemfundisha.
Huwezi kufahamu kesho utamkuta wapi yule uliyemfundisha na atakusaidia kwa njia gani. Hivyo kufundisha wengine hujenga kumbukumbu nzuri na ya kipekee.
Neno la mwisho
Kwa hakika huwezi kufahamu umuhimu au faida za kufundisha wengine ikiwa hujaanza kufundisha bado. Mimi mwenyewe awali nilikuwa nawaza kuwa nina mambo machache sana ya kuwafudhisha wengine, lakini baada ya kuyaweka kwenye mpangilio mzuri nimeona yakipokelewa vizuri sana na kuleta matokeo mazuri.
Hivyo ikiwa una maarifa fulani basi usisite kuyatoa kwa wengine ili wote mnufaike. Unaweza kufundisha kupitia mitandao ya kijamii, blog au hata ana kwa ana.
Je wewe huwa unafundisha wengine kwa njia moja au nyingine? Je unanufaikaje?

Post a Comment

0 Comments